Saturday 17 March 2012

ULUMWENGU WA MAENDELEO

Kola Friary - Morogoro

ULIMWENGU WA MAENDELEO:

Waswahili wana methali isemayo kwamba, "Mtaka cha uvunguni sharti ainame". Methali hii haitofautiani sana na ile isemayo kuwa; "Mchumia juani hulia kivulini".  Katika methali hizi za Kiafrika ndani yake tunapata falsafa ya Kiafrika inayotudhihirishia kwamba, mafanikio yoyote hayaji pasipo kujishughulisha. Hivyo ili mtu yoyote awezekufanikiwa katika ulimwengu huu hanabudi kujishughulisha ipasavyo. 
Lakini jambo la kushangaza sana kama siyo kusikitisha, vijana wengi wa Kiafrika hususani wa Kitanzania wamekuwa wakipuuzia mambo mbalimbali ambayo kwa namna moja au nyingine yangeweza kuwaletea mafanikio makubwa sana katika maisha yao. Nasema haya kwa uchungu sana kwani, nasikitika sana ninapowaona vijana wengi wakijishughulisha na upigadebe, ubwiyaji unga na uvutaji bangi. Mbaya zaidi siku hizi vijana wengi si wakike si wakiume wote wanashadidia mambo ya kipuuzi kama vile UDAKU. Hebu ni ulize, huenda labda mimi ndiyo mjinga!, Ulishawahi kusikia wapi mtu kafanikiwa kutokana na udaku!?
Wenye hekima na busara watakubaliana nami kwamba, asilimia kubwa ya magazeti ya udaku yanaandika habari zisizoleta maandeleo yoyote katika jamii zaidi ya kubomoa jamaii na kupandikiza ujinga katika kizazi kijacho. Hii imejidhihisha hata katika mitihani ya kidato cha nne mwaka huu kwani, watoto wengi wameshindwa kujibu vyema si kwa sababu ya magazeti ya udaku tu! hapana, bali kutokana na kwamba wanachokumbuka zaidi na walichoshika zaidi ni bongo flava na matusi ambayo kwa kiasi kikubwa ninaweza kusema wamejifunza kutoka katika magazeti hayo yasiyo na mbele wala nyuma.
Ukijaribu kufikiria japo kwa akili ya kawaida, mzazi anayesoma magazeti ya udaku nyumbani kwake, je watoto wake watakuwaje? Sijui! Hapa lazima tufike mahali na kujiuza kuwa Ulimwengu wa mafanikio ni upi? Je ule unaondekeza uvivu, utumiaji madawa haramu kama vile bangi na mengineyo, au udaku? 
Siku zote naamini kwamba akili iliyosafi na yenye fikra sahihi ni ile isiyofungamana na mambo yoyote yanayokwenda kiyume nayo. Hii ina maana kwamba mtu yoyote anayependa masuala ya udaku daima akili yake imejaa mambo kama hayo tu, na inapofika wakati wa kuchangia hoja za msingi kwa ajili ya mstakabali wa maisha yake au Taifa kwa ujumla anakuwa hana chochote cha kuchangia kutokana na kwamba akili yake haina kitu tofauti na udaku au umbea.
Naendele kusikitika sana hasa ninapowaona vijana wa Kichana jinsi walivyoingia kwa fujo katika nchi yetu. Tunaona sasa zile kazi ambazo zilikuwa zikifanya na vijana wa Kitanzania sasa zinafanywa na vijana wa Kichana. Kama huamini tembelea katika soko letu kuu KARIAKOO. Vijana wengi wa Kichina wameingia katika biashara ndogondogo yaani UMACHINGA biashara ambayo hapo zamani kwa kiasi kikubwa ilifanywa na vijana wa Kitanzania lakini sasa kutokana na ujio huu mtukufu Vijana wa kitanzania wameamua kuwapisha na kuhamia kwenye UPIGADEBE! 
Hofu yangu ni kwamba, China sasa inakuja juu sana kwa masuala ya sayansi na teknolojia, jambo hili halina mjadala kwani kila mmoja anashuhudia kwa macho yake jinsi Tanzania ilivyotekwa kwa bidhaa za Kichina. Achiliambali bidhaa hizo, sasa kuna magari chungunzima ya Kichina, mpaka daladala zetu. Sasa usije ukaona ajabu kusikia kuwa daladala za kutoka Mbagala - Ubugo zina dereva wa kichina, konda pamoja na wapigadebe. Hili si jambo la kuchekesha ni jambo la kusikitisha mno, maana huko ndiko tunakoelekea. 
Watanzania wenzangu! Uvivu, Burudani, Uzembe, Udaku vinatumaliza. Sina maana kwamba tusijihusishe na burudani. Hapana! Ila tunapaswa kuwa na kiasi kwa kuzingatia nafasi zetu na nyadhifa tulizokabidhiwa. Hapa sipendi kabisa kuzungumzia suala la MPIRA kwani hapa ndipo ugonjwa wa Watanzania wengi ulipojificha. "Manchester United, Madrid, Man City, Barcelona, Arsenal na nyingine nyingi." hahahahaahah! Ni jambo zuri na inashauriwa na wataalamu wetu wa afya kujiburudisha baada ya kazi ili akili iweze kupata nafasi ya kufikiri tena. Lakini tuangalie namna tunavyojipunzisha, je tunastahili mapumziko ya aina hii? Je kazi tulizofanya na kipato tulichopata kinaendana na burudani hizo?
Nadhani soka la Ulaya tukiliangalia kwa jicho yakinifu kwa kiasi fulani tunaweza kuona ni jinsi gani lilinavyochangia vijana wengi kuwa na maisha mazuri kama siyo mabaya. Samaha kama nitawakera kwani huu ni mtazamo wangu na nina kila sababu ya kusema hivyo kutokana na jinsi ninavyoona. Nasema hivyo kwa sababu moja kubwa, wenzetu wa Ulaya suala la michezo kwa ujumla ni jambo la ziada yaani hufanya kama sehemu ya mapumziko na fedha nyingi zinazotengwa katika michezo ni fedha za ziada "surplus".
Hii tunaona hata katika historia ya Riwaya na Tamthiliya tunaambiwa kwamba Chimbuko la fani hizi lilisababishwa na fani za kijadi pamoja na msukumo wa kijamii. Katika msukumo wa kijamii hapa ni pale ambapo tabaka la MABWANYENYE lilipoona kwamba linafedha nyingi na za kutosha liliamua kutafuta kitu cha kuwaburudisha na kuwastarehesha, hivyo mojawapo ikawa ni Fasihi. Hata katika mpira hali ilikuwa hivyo hivyo, kwani huwezi kujiburudisha kama huna kitu.
Hii ndiyo hali ya Tanzania ya leo ambayo bado inatawaliwa kifikra na mataifa ya Ulaya hata katika michezo mbalimbali. Hivi kweli wazungu wametufunga akili au tumejifunga wenyewe?
Hahahahahahah! Inafurahisha sana kuona wazungu jinsi wanavyotufundisha hata kuacha pombe. Yaani hata hili tunafundishwa! Kama unabisha sikiliza redio utasikia, "ULEVI NOOMA" TANGAZO HILI LIMEFADHILI NA WATU WA..... Si jambo la kucheka ni aibu! Usishangae sana maana waswahili wanasema kwamba,"Ukistaajabu ya Musa.....". Katika ndoa sasa, hapa ndo vituko kabisa kuona jinsi mama zetu na baba zetu wanavyofundishwa namna ya kuishi! Utasikia wanatuambia, "Vunja ukimya, sema naye" TANGAZO HILI LINAFADHILIWA NA WATU WA.....".
          HUU NDIYO ULIMWENGU WA MAFANIKIO NA TANZANIA YA KESHO

No comments:

Post a Comment