Tuesday 12 November 2013

MOTIFU YA SAFARI


MOTIFU YA SAFARI NA MSAKO KAMA MWEGA MKUU WA DHAMIRA KATIKA “MARIMBA YA MAJALIWA”
“Marimba ya Majaliwa ni hadithi iloyoandikwa na Edwini Semzaba mwaka (2008) ambayo inaelezea kuhusiana na marimba ya Majaliwa iliyopotea. Mwandishi ameonyesha jinsi Majaliwa alivyokuwa anatafuta marimba yake mpaka akaipata. Majaliwa alisafiri kwa kutumia njia mbalimbali kama vile ungo, fagio, na maumbo ya samaki akizunguka Tanzania nzima akisaka marimba ya nyuzi ishirini (20). Alianza Mafia, akaenda Zanzibar, Tanga, Moshi na Arusha, Iringa, Mwanza, Kigoma, na miji mingine mingi. Na Kongoti bingwa wa Taifa wa Marimba akimchenga kila mara huku akinga’nga’nia Marimba ya Majaliwa ili amzuie kushinda na ashinde yeye na bila Marimba yenye nyuzi ishirini (20) hakuna ushindi.

Katika mada hii tutaanza kuelezea maana ya fasihi, fasihi ya watoto, na maana ya motifu, na maaana ya dhamira. Kisha katika kiini cha swali letu tutachambua motifu mbalimbali  za safari na msako kama zilivyo jitokeza katika kitabu. Baada ya hapo kuonyesha dhamira mbalimbali.
Wataalamu mbalimbali wameelezea maana ya fasihi. Mulokozi (1996:3) akimnukuu Egletoni (1983:20-21), anasema fasihi ni sanaa ya lugha yenye ubunifu bilakujali kama imeandikwa au laa.
Mulokozi mwaka (1996), anasema ni sanaa ya lugha inayoangalia maisha na mazingira halisi. Anaendelea kusema kuwa ni sanaa ya lugha yenye ufundi wa hali ya juu ili kuweza kuwasilisha mawazo aliyonayo mtu kwa njia inayoweza kuathiri kwa kutumia sanaa hiyo  kimaandishi au  kimazungumzo.
TUKI (2004), wanasema mtoto ni mtu mwenye umri mdogo, katika maana hii hajatueleza umri huo ni wa kuanzia miaka mingapi hadi miaka mingapi lakini kutokana na maana hii Mulokozi (2008:338), anasema fasihi ya watoto na vijana ni ile fasihi inayorejelea matini au kazi ambazo kimsingi hadhira yake ni watoto na vijana, na hii ni kati ya umri wa miaka 0-10 na 11-17. Hivyo fasihi ya watoto na vijana huhusisha kazi zinazowahusu bibadamu kati ya miaka 0-17. Na kazi hizo zaweza kuwa riwaya, Hadithi fupi, Tamthilia au Ushahiri.
Motifu- Ni dhana/jambo au kipengele kinachojirudiarudia katika kazi ya fasihi. Ambacho kinaweza kuwa cha kifani au kinaudhui. Mfano; Motifu ya safari.
TUKI (2004), dhamira ni kiini cha jambo au habari iliyosimuliwa ama kuandikwa hasa katika fasihi
Madumulla (2009), Dhamira ni wazo kuu katika kazi ya fasihi. Kwa ujumla wote wanazungumzia jambo au  wazo kuu katika fasihi, Hivyo tunakubaliana na fasihi zote hapo juu.
Kuanzia mwanzo hadi mwisho wa kitabu tunaona Majaliwa alisafiri sehemu mbalimbali hadi kufikia kiwango cha kuzunguka nchi nzima huku akimsaka Kongoti ili aweze kuirejesha Marimba yake. Safari ya Majaliwa ilianzia Mafia mkoani Pwani. Hii ni baada ya kuchukuliwa Marimba yake na watu ambao awali hakuwafahamu na baadaye walikimbia kichakani (ukurasa wa 2). Kwa kuwa marimba nguvu zake ziliambatana na nguvu ya kuzimu, usiku wa manane marehemu bibi yake mzaa mama alimjia ndotoni na kumwambia Majaliwa kuwa, Kongoti Nachienga ndiye aliiba Marimba yake kwa wasiwasi wa kushindwa wakifika Dodoma kwenye mashindano ya marimba ya kitaifa. Katika upande wa kuzimu babu yake Majaliwa mzaa baba yake yupo upande wa Kongoti (ukurasa 3)
Safari ilianza rasmi usiku wa manane kisiwa cha Mafia katika ufukwe wa kilindoni wa Bahari ya Hindi. (uk.5). Walisafiri huku bibi yake akiwa katika umbo la samaki (nguva na papa) (uk.5) hadi Zanzibar (uk.7-10). Akiwa huko Majaliwa aliendelea kumsaka Kongoti bila mafanikio (uk.11). Majaliwa anaendelea na safari kuelekea Tanga. Wanatumia aina mbalimbali za usafiri kama Ungo, Ufagio, Chai maharage, na basi mfano (uk.21,22 na 105). Majaliwa anakumbana na misukosuko mbalimbali baharini hatimaye anafika Tanga, lakini juhudi zake hazimpi mafanikio (sura ya 7-11). Majaliwa baada ya kusikia kwamba Kongoti alikuwa anaelekea Kilimanjaro alianzisha safari ya kuelekea huko ili aweze kuitwaa marimba yake sura ya (11-17) kwa usafari wa basi (uk.46). Kutokana na misukosuko mbalimbali Majaliwa anachelewa. Kilimanjaro alikuta mashindano yamekwisha na Kongoti sasa anaelekea Arusha. Majaliwa naye ili kuisaka marimba yake aliamua kumsaka Kongoti lakini pasipo na mafanikio yoyote.
Baadaye Majaliwa alisafili kwenda Singida (sura 26-27) baadaye Kondoa kwenda Tabora (sura ya 27-30) Pia Tabora kwenda Shinyanga. Katika safari zote hizo Majaliwa hakufanikiwa kutwaa marimba yake lakini hakukata tamaa aliendelea na safari ya msako ukurasa 239.
Majaliwa anaendelea na safari kutoka Shinyanga kwenda Mwanza baada ya kufika alishuka kwenye ndege na kupanda daladala kuelekea Mwanza (uk.131) baada ya hapo Majaliwa alisafiri kuelekea Butihama baadaye kurudi Mwanza kwa kujionea maeneo mbalimbali ya kihistoria (uk.138-140) Wakiwa katika usafiri wa meli Majaliwa alivamiwa na Kongoti. Akapambana naye ili airejeshe marimba yake lakini Marimba ile ilitumbikia ziwani (uk.141) Bibi yake alipotokea akamwelezea kisha akayafuatilia na kumwambia kuwa hayakuwa yenyewe. Wakatembelea sehemu mbalimbali za kihistoria za Mwanza meli ilifika Kemondo Bukoba kagera ambapo palikuwa na mashindano pia na Kongoti angekuwa miongoni mwao alisafiri sehemu mbalimbali za karagwe kwa basi kutokana na ulinzi mkali aliondoka kutembelea sehemu mbalimbali za kihistoria (uk.151)
Majaliwa aliendelea na safari ya kuelekea Kigoma (uk.155) ambapo alitembelea sehemu mbalimbali za vivutio vya watalii baadaye mashindano yalifanyika hoteli ya Lake Tanganyika ambapo alipata nafasi ya kufanya ufunguzi na hakupata pesa nyingi hapo usiku walisafili kwa ungo kupitia Mbozi na milima ya mrengi baadaye Mbeya ambapo mashindano yalifanyika Kileleni lodge ambapo alitumia njia mbalimbali na kuipata marimba lakini haikuwa yenyewe (uk.175) safari ya usiku ilikuwa ni kutembelea maeneo mbalimbali ya kihistoria kuamkia Iringa ambapo Kongoti angetumbuiza kwenye maadhimisho ya shujaa Mkwawa (uk.187) Baadaye Kidatu Njombe, Rudewa hadi Manda. Baadaye Mji wa Tunduma Mola tena Mwanjerwa alisikia Kongoti bado anapiga marimba aliamini kuwa bado ana marimba yake (uk.197)
Safari ya Majaliwa huko Mbeya kwenda Songea kwa basi la Scandinavia (uk.198) Mashindano ya Ruvuma Lindi na Mtwara, pia wakiwa Ruvuma walitembelea sehemu mbalimbali za kihistoria (uk.200-205), Baadaye Ndanda, Newala, Mtwara, Mnazi bay, Lindi (Tengeru) (uk.205) Baadaye ukumbi wa mkorosho mpya ambapo mashindano yalifanyika lakini majaliwa hakupata nafasi ya kumsogelea Kongoti (uk.208) kwa usafiri wa Ufagio walienda Rufiji hadi Mafia, Mkuranga, Dar es salaam, Temeke, Mwenge, Lugalo, Bagamoyo na sehemu mbalimbali za Dar es salaam (uk.211).
Kutoka Dar Es Salaam alifunga safari yake hadi Morogoro (uk.212) kwa usafiri wa basi baada ya kupita sehemu mbalimbali Majaliwa alifanikiwa kuikuta Marimba Mjini Morogoro akiwa katika harakati za safari ya kuelekea katika shindano la kitaifa huko Dodoma ilikuwa baada ya kubadilisha marimba katika sinia la ukaguzi hapo tena Majaliwa alianza kujiandaa kusafiri kwa basi kwenda Dodoma kwenye mashindano ya kitaifa pamoja na misukosuko ya kukatika kwa daraja (uk.230) Baadaye aliingia Dodoma kwa kupitia Chamwino Dodoma Mjini baadaye Milimani ambapo mashindano yalifanyika hoteli ya Milimani huko Dodoma na kuibuka Mshindi wa kuwabwaga wenzake wote pamoja na adui yake Kongoti na kukamilisha ndoto zake za kuwa bigwa wa Taifa.
Maana ya ujasiri Kwa mujibu wa TUK (2004), hali ya kukabili jambo hofu uhodari na ushujaa. Ujasiri ni dhamira kuu katika kitabu hiki ambayo imejitokea katika motifu zote na misako ambayo imeandikwa katika kitabu hiki Majaliwa ameonesha kuwa jasiri kuanzia mwanzo wa hadithi pale anapoanza kutafuta marimba yake iliyoibwa akisaidiwa na bibi yake. Hili limeonekana katika sehemu mbalimbali mfano:- katika ukurasa wa 72 sura ya 17 ambapo majaliwa anapambana na dereva taski baada ya kutaka kumwibia majaliwa pesa zake wakati wakimtafuta kongoti aliyekuwa kwenye pikipiki.
“Majaliwa akiwa ameshika jiwe lake la rubi alimpiga nalo Yule dereva kwenye macho yake yote mawili mara mbili”
Mfano mwingine ni pale majaliwa alipopambana na kongoti mlenzi wakinyang’anyana marimba majaliwa alikuwa mtoto mdogo lakini aliweza kukabiliana na kongoti ambaye alikuwa mtu mzima. Hili limeoneshwa katika ukurasa wa 141 sura ya 34.
Nalianza kukamatana na kuangushana na ingawa alikuwa mtoto tu, uchungu wa kudhulumiwa marimba yake ulimjaza ari na akachuana kishujaa”  
Hivyo basi kwa kuangalia hiyo mifano tunaona majaliwa alikuwa jasiri na mwandishi alionesha hili kama dhamira kuu
Dhamira nyingine ni Imani za kishirikina. Imani kwa mujibu wa Kamusi TUKI (2004), ni mambo anayoyakubali mtu kuwa ni ya kweli na anayopaswa kuheshimu, haswa katika dini, au itikadi. Ushikirina ni tabia ya kuamini mambo ya uchawi, mizimu, nk. Katika kitabu hiki dhamira ya imana ya kishirikina imejijenga sana katika motifu ya safari na msako iliyojitokeza katika kitabu hiki mfano katika kitabu hiki mwandishi alionyesha hili pale majaliwa alipokuwa anasafiri kwa njia ya kishirikina kama vile ungo, fagio, pia kuna wakati mwingine alikuwa anasafiri kutoka sehemu moja kwenda nyingine kwa kufumba macho na kufumbua. Mfano mwingine ni ule kusafiri kwa ungo imeoneshwa (uk.52), Bibi alimwambia Majaliwa apande kwenye Ungo.
“ Bibi alimwambia mjukuu wake sasa na wewe panda kwenye ungo” .
 Pia kusafiri kwa ufagio (uk.105) Majaliwa alimletea bibi fagio uliokuwa umeachwa kwenye takataka. “Haya panda nyuma” Kufumba na kufumbua wakajikuta wako angani.
Dhamira nyingi ni Rushwa. Rushwa ni fedha au kitu cha dhamani kinachotolewa na kupewa mtu mwenye madaraka ya kitu fulani ili mpaji apatiwe upendeleo. Katika kitabu hiki rushwa ilijitokeza pale ambapo Majaliwa alimpa fedha kwa sababu hakuwa na kibali cha kuingia sehemu za utalii ili aweze kumwachia. Hili limeoneshwa uk.66
“Majaliwa alipoangalia saa iliyotundikwa ukutani na kuona ni saa tano, alibadilisha uamuzi wake na kuongeza dola moja, hapo askari hakusema kitu”.
Hilo pia limeoneshwa katika uk.213 sura ya 54.
 Tamaa ni hamu kubwa ya kupata kitu au shauku au matarajio ya kupata kitu. Hili mwandishi pia amelibainisha kwa kuanza na Majaliwa ambaye yeye  alikuwa na tamaa ya kupata marimba yake iliyochukuliwa na kongoti kiasi cha kuamua kujitosa na kuanza kutafuta kwa kupitia hali  mbalimbali ingawa alikuwa ni mtoto. Tamaa pia imeoneshwa pale ambapo dereva teksi alitamani dola za Majaliwa alipokuwa anamwendesha mpaka akapata upofu kwa kupigwa na Majaliwa. Pia bibi alihadithia hadithi moja ambayo ilikuwa inaonyesha jinsi ambavyo tamaa ni mbaya uk.123-126.
“Bibi akamuuliza Majaliwa hadithi inakufundisha nini? Majaliwa anajibu Tamaa ni mbaya”. Katika uk.72 dereva teksi aliona pesa za majaliwa na kuzitamani hivyo akampeleka porini. Dereva anamwabia, “toa pesa zote ulizonazo haraka”
Madhara ya kutokuwa mtiifu. Hili pia mwandishi amelionesha katika kitabu chake pale ambapo Majaliwa alikuwa anakiuka maagizo ambayo alikuwa anapewa na bibi yake na kupata madhara. Hili mwandishi amelionesha katika uk.50 ambapo bibi anamwambia majaliwa.
 siku zote utii ni bora”. ‘Si nilikukataza kula kitu chochote kupitia kinywani” Hapo ndipo Majaliwa akakumbuka alikula mayai kwenye tumbo la nyangumi.  Bibi akasema “hilo ndilo kosa ndio maana Rubi haikufanya kazi yake nami nikakupa adhabu ya kuwa peke yako usiku wote wa jana.
Pia Bibi alimwadithia Majaliwa Hadithi ya madhara ya kutokuwa mtiifu katika uk.169-171 ambayo ikimuelezea mvuvi ambaye alikosa utiifu na mwishowe akakosa utajiri kwa ajili hiyo.
Dhamira nyingine ni ile ya umuhimu wa kujua historia mbalimbali ya maeneo katika nchi. Hili mwandishi amelionesha wazi kwani limeoneshwa na kujengwa dhamira na motifu ya safari kwani katika safari ambazo Majaliwa alizifanya ndipo hapo aliweza kujua historia za sehemu mbalimbali alizosimuliwa na bibi yake. Kwa ujumla kulikuwa na hisoria ya mapango ya Amboni Tanga, Kondoa Iringa, mji wa Tabora, hisotria ya ngome kongwe, Kaburi la Abeid Amani Karume, Wangoni. Makaburi ya watu waliokufa kwa ajili ya Treni, Meli iliyozama ya MV Bukoba na sehemu nyinginezo.
Pamoja na kuwepo na dhamira hizo hapo juu zilizoelezwa kwa mapana na marefu kulikuwepo pia dhamira nyinginezo ambazo zilizokuwepo katika kitabu hiki. Dhamira hizo ni pamoja na wizi, wivu, mashindano, kujikinga na ukimwi, chuki, nafasi ya mwanamke katika jamii, Ukombozi, Elimu, Ukatili, Umoja na mshikamano na hali ngumu ya maisha. Hivyo kwa ujumla tunaweza kusema kuwa mwandishi amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kujadili masuala mbalimbali yaliyoko katika jamii hasa jamii yetu ya Kitanzania.

 MAREJEO
Madumulla, S. (2009), Riwaya yaKiswahili: Mature Educational Publishers Lited.
Mulokozi, M. M. (1996), Utangulizi wa Fasihi ya Kiswahili: Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili, Dar es Salaam.
Semzaba, E. (2008), Marimba ya Majaliwa. E&D Publishers Limited:Dar Es Salaam.
TUKI (2OO4), Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Taasisi ya Taaluma za Kiswahili: Dar Es Salaam.

No comments:

Post a Comment