Sunday 17 November 2013

HADITHI

       MAJUTO NI MJUKUU  

Hapo zamani za kale, hapa kwetu kijijini,
Kijiji kilo vutia, pande zote za dunia,
Walifurika wageni, maajabu jionea,
Masikini mwananchi, majuto ni mjukuu.

Ardhi yenye madini, mito mbuga za wanyama,
Viumbe wa maajabu, mlima wenye theluji,
Maziwa yalofurika, viumbe kila aina,
Maskini mwananchi, majuto ni mjukuu.


Ardhi ilo bikira, kila kitu ya chipusha.
Haikupita masika, bila mbingu kufunguka,
Vilindini makondeni, mifugo ya sherekea,
Masikini mwananchi, majuto ni mjukuu.

Akaibuka kijana, akanadi zake sera,
Wote tukashawika, kura tukammwagia,
Tukidhani yu masiha, duniani ameshuka,
Jambo usilolijua, kama usiku wa kiza.

Hata ukimtazana, shaka huna juu yake,
Tabasamu limejaa, hii ndiyo jadi yake,
Wazee walimpenda, wake pia wasichana,
Jambo usilolijua, kama usiku wa kiza.

Mambo yakawa majambo, shilingi kaigeuza,
Nyerere kaenda nyuma, swala wakaenda mbele,
Madukani wakataa, wadai haina hadhi,
Jambo usilolijua, kama usiku wa kiza.

Kaanza kama mzaha, aridhi kamegamega,
Kagawa huku na huku, hata vijiji vya ng’ambo,
Wageni kawabatiza, waitwa wawekezaji,
Masikini wananchi, majuto ni mjukuu.

Aridhi wakachimbua, wakaokota johari,
Mapango yakatokea, tukaita makumbusho,
Macho ya baki angani, twashangaa wapepea,
Masikini wananchi, majuto ni mjukuu.

Maandamano popote, utadhani kumbikumbi,
Bibi mbele bwana nyuma, tunadai chetu kitu,
Mabomu yaturudisha, ulinzi kila mahali,
Masikini wananchi, majuto ni mjukuu.

Wazee hawaamini, kile wanachokiona,
Wamekuwa wakimbizi, ndani ya kijiji chao,
Vijana wameduwaa, wamebaki njia panda,
Masikini wananchi, majuto ni mjukuu.

Kila mwezi luningani, kila siku gazetini,
Kila saa redioni, vipeperushi kutani,
Maisha bora kwa wote, umekuwa wimbo wake,
Jambo usilolijua, kama usiku wa kiza.

Bora nijinyamazie, niepuke mabwepande,
Viungo nikapoteza, nikabaki taabika,
Maisha haya magumu, hata upake siagi,
Jambo usilolijua, kama usiku wa kiza.

Jamani kosa si kosa, kosa kurudia kosa,
Hili sote tunakiri, kosa tumelirudia,
Rabuka tuhurumie, nyoosha wako mkono,
Jambo usilolijua, kama usiku wa kiza. 

 Hadithi nimemaliza, koo limenikauka,
Mjukuu nipe maji, niburudishe mtima,
Fundisho umelipata, usije nawe jutia,
Jambo usilolijua, kama usiku wa kiza.

No comments:

Post a Comment